SIKU KUMI ZA MWEZI WA DHUL HIJJAH


USIPITWE NA FURSA HII: Anasema mtume wa Allah rehema na amani ziwe juu yake, (Hakuna siku ambazo matendo mema ndani yake ni yenye kupendezwa zaidi mbele ya Allah kulikoni Siku hizi (siku kumi za mwezi wa Dhul Hijja) Maswahaba wakauliza: Ewe mtume wa Allah: Wala Jihadi kwa ajili ya njia ya Allah?
Akawajibu: Wala jihadi kwa ajili ya njia ya Allah, Isipokuwa kwa yule mtu aliyetoka na nafsi yake na mali zake kisha kikawa hakijarudi chochote katika hivyo (nafsi na mali). Hadithi imesimuliwa na Ibun Abbasi radhiya Allahu anhumaa na kupokelewa na Abu Dawud na Ibn Majah.
JE MATENDO HAYO YANAYO PENDEZWA KUYAFANYA NDANI YA SIKU HIZI NI YAPI?
  1. KUFANYA IBADA YA HIJJAH NA UMRA: Kama anavyo tueleza Mtume rehema na amani ziwe juu yake: (Ibada ya umra mpaka ibada ya umra ni kifutio cha madhambi yaliyo kati yake, na ibaada ya hijja iliyo kamilisha nguzo zake na masharti yake, haina malipo isipokuwa pepo) 
  2. KUFUNGA SIKU HIZI ZOTE TISA AU KADIRI YA UWEZO KHUSUSANI SIKU YA TISA SIKU YA ARAFA: Bila shaka ibada ya swaumu ni katika ibaada zenye thawabu mbele ya Allah Azza Wajalla na katika hadithi zilizokuja kuelezea umuhimu na fadhila za swaumu ni hadithi hii ya Mtume salla Allahu alayhi wasallam: (Mwenye kufunga siku moja kwa ajili ya Allah basi Mwenyezi Mungu utauweka uso wake mbali na moto wa jahanamu muda wa miaka sabini) Na kuhusiana na fadhila za kufunga siku ya Arafa mtume anatueleza ya kwamba: (Funga ya siku ya Arafa ninatarajia Allah atawafutia waja madhambi ya mwaka ulio pita na mwaka ujao) 
  3. Kuzidisha adhkari: Nyiradi mbali mbali katika siku hizi kumi, kama vile Takbira (ALLAHU AKBARU:Mungu mkubwa) ALHAMDULILLLAHI: Shukurani zote anastahiki Mwenyezi Mungu. ISTIGHFARI: Kumtaka msamaha Mwenyezi Mungu. Na mfano wa hizo katika adhkari zilizo pokelewa katika mwongozo wa mtume wetu Muhamadi rehema na amani ziwe juu yake. 
  4. KUTUBIA KWA ALLAH NA KUJING`OA KUTOKA KATIKA MAASI YOTE. Kwani utiifu (Kumtii Allah) ni katika sababu za kumfanya mja awe karibu na Allah na maasi au madhambi ni katika mambo yanayo muweka mja mbali na Allah. Na toba ni katika mambo yanayo mfurahisha Allah. 
  5. KUZIDISHA KUFANYA MAMBO YA KHERI: Kama vile kuswali swala zote kwa nyakati zake. Vile vile kuzidisha ibaada za suna na kutoa sadaka na kuamrishana mambo mema, kukatazana maovu na kadhalika
  6. KUCHINJA SIKU YA IDDI EL ADH-HA: Kwa kumuiga kigezo chetu na mtume wetu Nabii Ibrahimu alayhi salaam. Na mtume wetu Muhammad rehma na amani ziwe juu yake. Ibada hii ya kuchinja ni ibaada ya sunna na wanyama wanao faa kuwachinja ni ngamia, ng`ombe, mbuzi na kondoo. Ngamia au ng`ombe wanaweza changia watu saba, ama mbuzi na kondoo ni kwa mtu mmoja tu. Mnyama huyu inapaswa asiwe na kasoro kama vile uchongo upofu na kilema. 
  7. KWA MWENYE KUTAKA KUCHINJA NDANI YA SIKU YA IDDI: Basi ni sunna kwa mtu huyu asinyoe nywele zake na kukata kucha zake mpaka siku ya kuchinja.
  8. KUJITAHIDI KUSWALI IBADA YA SWALA YA IDI: Kwani ibaada hii kwa mwaka ni mara moja tu,kwa hiyo ni muhimu kujitahidi kutekeleza ibaada hii.